.

.

.

.

Monday, January 26, 2015

BARAZA JIPYA LA MAWAZIRI KUFUATIA SAKATA LA ESCROW




Rais Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko 13 kwenye Baraza la Mawaziri yaliyohusisha mawaziri nane, manaibu watano, wakiwamo wapya wawili, ikiwa ni siku mbili kabla ya kuanza kwa Bunge.
Rais pia aliwaapisha mawaziri wote 13 akiwamo waziri mpya wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe ambaye alisababisha hafla hiyo kuchelewa kwa kuwa alikuwa akitokea Davos, Uswisi.
Mabadiliko hayo, yanayoweza kuwa ya mwisho kwa Rais Kikwete, yamefanyika ikiwa imesalia miezi sita kabla ya kuvunjwa kwa Bunge kupisha Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba.
Rais amelazimika kufanya mabadiliko hayo baada ya mawaziri wawili, Profesa Anna Tibaijuka na Profesa Sospeter Muhongo, kuondoka kutokana na kuhusishwa na kashfa ya uchotwaji fedha kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, ambayo pia imesababisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliackim Maswi kusimamishwa kazi, huku waziri wa zamani wa wizara hiyo, William Ngeleja akivuliwa uenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria.
Kwa mujibu wa mabadiliko hayo, Kikwete amewaondoa mawaziri wawili wazoefu kutoka Ofisi ya Rais, Steven wasira na Ofisi ya Waziri Mkuu, William Lukuvi, kuwapangia wizara nyingine, huku akimhamishia Dk Mary Nagu kwenye Ofisi ya Rais na Jenister Mhagama (Waziri Mkuu).
Akitangaza mabadiliko hayo juzi, Katibu Mkuu Kiongozi Ombeni Sefue alisema mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene, ambaye alikuwa naibu wa wizara ya Nishati na Madini kuanzia mwaka 2012 hadi 2014 na ambaye  alikuwa naibu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ameteuliwa kumrithi Profesa Muhongo kwenye wizara hiyo tata ya Nishati na Madini.
Simbachawene anakuwa waziri wa nne kushika wizara hiyo tangu Serikali ya Awamu ya Nne iingie madarakani na anaingia wakati Steven Masele, aliyekuwa naibu Waziri wa Nishati na Madini, akiwa amehamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano). Nafasi ya Masele imechukuliwa na mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage ambaye ameteuliwa kwa mara ya kwanza.
Sefue alisema mbunge wa Ismani, William Lukuvi, ambaye tangu mwaka 2010 amekuwa Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Utaratibu na Bunge), ameteuliwa kuziba nafasi ya Profesa Tibaijuka ya uwaziri wa Kazi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Sura nyingine ngeni kwenye baraza hilo, kwa mujibu wa Sefue, ni ya mbunge wa Same, Anne Kilango Malecela, mmoja wa wazungumzaji wakubwa bungeni, ambaye ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Elimu.
Alisema aliyekuwa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama amepanda kuwa Waziri wa Nchi, Sera, Uratibu na Bunge, nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Lukuvi.
Nagu amehamia Uhusiano na Uratibu (Uwekezaji na Uwezeshaji) na Dk Harrison Mwakyembe anayehamia Afrika Mashariki (Uchukuzi).
Wengine ni mwanasiasa mkongwe, Steven Wasira aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Kilimo akitokea Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, wakati Samuel Sitta anakwenda Uchukuzi akitokea Wizara ya Afrika Mashariki
.

No comments:

Post a Comment